Monday, September 7


Ligi Kuu Tanzania Bara msimu wa 2015/16 inaanza mwishoni mwa wiki hii Septemba 12 na itashirikisha timu 16 zitakazokuwa zimetoka mikoa tisa tofauti huku zikicheza kwenye viwanja 13 tofauti.
Timu hizo ni bingwa mtetezi Yanga, Simba, Azam, Kagera Sugar, Mtibwa Sugar, JKT Ruvu, Mwadui FC, Coastal Union, African Sports, Majimaji, Toto Africans, Mgambo Shooting, Mbeya City, Tanzania Prisons, Ndanda FC na Stand United.
Viwanja vitakavyotumika ni: Taifa, Nangwanda, Mkwakwani, Majimaji, Azam Complex, Kambarage, CCM Kirumba, Sokoine, Mwadui, Manungu, Jamhuri, Ali Hassan Mwinyi na Kaitaba.
1. Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam
Uwanja huu ulianza kutumika mwaka 2007.Una vipimo vya mita 105 kwa mita 68 na milango 35 kwa ajili ya mashabiki kuingia na kutoka uwanjani. Una uwezo wa kuchukua zaidi ya mashabiki 57,000 waliokaa.
Klabu zitakazoutumia Uwanja huu kama Uwanja wa nyumbani ni Simba na Yanga.
2. Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi, Tabora
Ulijengwa mwaka 1987 chini ya wakandarasi wa kampuni za Beco, Kamota na Natco, na unamilikiwa na Chama cha Mapinduzi (CCM).
Una uwezo wa kuchukua watazamaji 30,000 kwa wakati mmoja. Klabu itakayoutumia Uwanja huu kama Uwanja wake wa nyumbani ni Kagera Sugar ambao wameuhama Uwanja wa Kaitaba- Bukoba wakipisha marekebisho.
Hata hivyo Kagera Sugar watarejea Kagera mzunguko wa pili wa Ligi na kuendelea kuutumia Uwanja wao wa Kaitaba ambao ulijengwa mwaka 1957 na unamilikiwa na Manispaa ya mji wa Bukoba. Kaitaba una uwezo wa kuchukua watu 5, 000 kwa wakati mmoja.
3. Uwanja wa Kirumba, Mwanza
Uwanja wa Kirumba upo jijini Mwanza na unamilikiwa na Chama cha Mapinduzi (CCM).
Uwanja huu ulijengwa mwaka 1980 na una uwezo wa kuchukua watazamaji waliokaa 25,000. Uwanja huu utakuwa ukitumiwa na klabu ya Toto African ya Mwanza.
4. Uwanja wa Sokoine, Mbeya
Unapatikana katikati ya Jiji la Mbeya na ulijengwa mwaka 1977. Uwanja wa Sokoine una uwezo wa kuchukua mashabiki 21,000 na unamilikiwa na CCM.
Klabu ya Tanzania Prisons inayomilikiwa na Jeshi la Magereza na Mbeya City inayomilikiwa na Manispaa ya Mbeya zitautumia Uwanja huu kama Uwanja wa nyumbani.
5. Uwanja wa Majimaji, Songea
Uwanja wa Majimaji upo katikati ya mji wa Songea mkoa wa Ruvuma na unamilikiwa na CCM. Ulijengwa mwaka 1979. Uwanja huu una uwezo wa kuchukua watazamaji 18,000 na utakuwa ukitumiwa na timu ya Majimaji kama Uwanja wa nyumbani msimu huu.
6.Uwanja wa Mkwakwani, Tanga
Ulijengwa mwaka 1975 na Kampuni ya Amboni Plantation. Uwanja wa Mkwakwani una vipimo vya ukubwa wa mita 105 kwa mita 68, pia una milango saba na uwezo wa kuchukua watazamaji 15,000. Mmiliki wa Uwanja huu ni CCM. Klabu za Coastal Union, African Sports na Mgambo Shooting zitautumia Uwanja huu kama Uwanja wao wa nyumbani.
7.Uwanja wa Kambarage, Shinyanga
Uwanja huu upo Manispaa ya Shinyanga na ulianza kutumika mwaka 1985. Una uwezo wa kuingiza watazamaji 15,000.
Uwanja huu ulipewa jina la Kambarage kama njia ya kumuenzi Rais wa kwanza wa Tanzania, Mwalimu Julius Nyerere.
Kama vilivyo viwanja vingi, pia unamilikiwa na CCM, klabu ya Stand United itautumia kama Uwanja wake wa nyumbani.
8.Uwanja wa Nangwanda Sijaona, Mtwara
Uwanja huu upo katika Manispaa ya Mtwara eneo linalofahamika kama Umoja. Una uwezo wa kuchukua mashabiki 10,030 na una milango minne kwa ajili ya kuingia na kutoka uwanjani. Mmiliki wa Uwanja wa Nangwanda Sijaona ni CCM. Klabu ya Ndanda FC itautumia kama Uwanja wake wa nyumbani.
9.Azam Complex- Chamazi, Dar es Salaam
Ujenzi wake ulianza mwaka 2010 chini ya mkandarasi Kampuni ya Salehe Msahala Contractors Limited. Azam Complex una uwezo wa kuingiza watazamaji 7, 000.
Klabu zitakazoutumia Uwanja huu kama Uwanja wake wa nyumbani ni Azam na JKT Ruvu. Mmiliki wa Uwanja huu ni Azam.
10.Uwanja wa Mwadui, Shinyanga
Ulijengwa mwaka 2010.Uwanja wa Mwadui una uwezo wa kuchukua mashabiki 5,000.
Mmiliki wa Uwanja huu unaopatikana ndani ya eneo la migodini ni wa Kampuni ya Diamond Petra. Klabu ya Mwadui Fc itautumia kwa michezo ya nyumbani.
11.Uwanja wa Manungu, Morogoro
Uwanja huu ulijengwa mwaka 1988 na una uwezo wa kuchukua watazamaji 4,000. Mmiliki wake ni kampuni ya Mtibwa Sugar. Klabu ya Mtibwa Sugar itautumia Uwanja huu kama Uwanja wake wa nyumbani, lakini itakapokabiriana na Simba au Yanga itatumia Uwanja wa Jamhuri Morogoro ambao ulijengwa mwaka 1978 na unamilikiwa na CCM. Jamhuri una uwezo wa kuchukua watazamaji 20,000.    

0 comments:

-