Monday, August 17

friendsKipindi cha nyuma kidogo niliwahi kuandika makala juu ya umuhimu wa kila mmoja kuwa na marafiki. Katika makala hayo nilisema wazi kwamba, kuishi bila marafiki ni tatizo na ukijaribu kufuatilia wale ambao hawana marafiki, maisha yao yana upungufu.
Nikashauri kwamba, ili maisha yako yakamilike ni vyema ukachagua marafiki ambao watakuwa ni wenye faida kwako. Lakini wakati nikishauri hivyo, wapo watu ambao naona wazi maisha yao hayana dira, wapo wapo tu kwa sababu ya aina ya watu ambao wamechagua wawe marafiki zao.
Unapochagua mtu wa kumfanya awe rafiki yako, ina maana umeona mnaendana katika mambo mbalimbali. Huwezi kumfanya mtu f’lani awe rafiki yako wakati unajua yeye ni mlevi na wewe si mlevi. Yeye ni mwizi, wewe hupendi kuwa hivyo! Ukiwa karibu na mtu huyo, ni rahisi sana kujiingiza huko.

 Ndiyo maana ukifuatilia sana utagundua vijana wengi wanaojifundisha tabia za wizi na uvutaji bangi walianza kwa kujiweka karibu na marafiki wenye tabia hizo. Hiyo ni ishara tosha kwamba, usipokuwa makini kwenye kuchagua rafiki, usishangae maisha yako yakawa mabaya, tofauti na vile ulivyokuwa unafikiri.
Nimelazimika kulizungumzia hili kwa sababu nimegundua wengi wetu tunashindwa kuyafikia mafanikio tunayotakiwa kuwa nayo kwa kuwa na marafiki wabaya ambao hugeuka kuwa vikwazo.
Hebu fikiria, unakuwa na rafiki ambaye siku zote pesa zake zinaishia kwenye anasa. Yaani kila ikifika mwisho wa mwezi anakushawishi muende kwenye kumbi za starehe, kunywa pombe kwa sana na mambo mengine ambayo yamekuwa yakiwarudisha nyuma wengi.
Kama ulikuwa hujui, rafiki uliyenaye ambaye hawazi mambo ya kimaendeleo anakuathiri kwa kiwango kikubwa sana. Yawezekana mafanikio uliyonayo leo yangekuwa mara mbili yake kama ungechagua marafiki wengine tofauti na hao ulionao sasa!
Ni wangapi unaowajua wewe ambao walikuwa si walevi kivile lakini baada ya kuwa na marafiki wenye hulka hiyo nao wakatopea huko? Ni wanawake wangapi unaowajua ambao huko nyuma walikuwa wametulia lakini baada ya kuwa na marafiki micharuko nao wakawa walewale?
Ni wengi sana ambao wameathiriwa na marafiki zao na hili linatokana na kutokuwa makini na aina ya watu wa kuwa nao karibu.
Wapo watu ambao wana aleji na mafanikio, wakipata pesa wao wanatumbua tu, wala hawafikirii kwamba kuna kesho. Hawa ni wale wanaoishi kwa kufuata ile misemo ya kijinga kama vile, tumia pesa ikuzoee au wale ambao kila siku wanafikiria kujenga heshima baa.
Hivi wewe ambaye unasoma makala haya unadhani ukiwa na rafiki wa dizaini hiyo utaweza kujitoa kwenye mawazo hayo? Hakika ni ngumu, labda Mungu akupe ujasiri wa kujinasua kutoka kwa marafiki wenye akili hizo finyu.
Ndiyo maana nasema, marafiki ni muhimu sana kwenye maisha yako lakini uangalie yupi anafaa na yupi ambaye ukiwa naye karibu atakulostisha!
Ni vyema leo hii ukawafanyia uchambuzi marafiki zako ulionao na kuangalia kama wamekuwa na faida au wamekuwa chanzo ya kuyafanya maisha yako yawe hayana mbele wala nyuma.

0 comments:

-