Saturday, January 24

Hali inatisha! Vidonge vinavyodaiwa ni vya kutoa mimba vimezagaa kwenye maduka ya madawa baridi ‘famasi’ jijini Dar na kuuzwa kinyume cha sheria iliyowekwa na wahusika kwa kuwa hairuhusiwi kuuziwa dawa hizo pasipokuwa na kibali cha daktari.

Wauzaji wa moja ya duka la dawa linalouza dawa za kutolea mimba.
Kikosi chetu cha Oparesheni Fichua Maovu (OFM) kiliingia kazini kuzisaka famasi zinazodaiwa kujihusisha na biashara ya dawa hizo zilizotajwa kwa jina la Misoprostol 200.
ENEO LA KWANZA

Zoezi lilianzia kwenye famasi za Mwenge, Dar (majina yanahifadhiwa kwanza) ambapo OFM walikwenda kwa lengo la kutaka kununua dawa hizo ambapo muuzaji wa kwanza ambaye ni mwanaume alikiri kuziuza kwa bei ya sh 10,000.


Kamanda wa OFM (kulia) akimbana kwa maswali mmoja wa wauzaji hao.
Katika famasi nyingine maeneo hayo, muuzaji wa pili aliiuza kwa  sh 25, 000 huku akikiri kuwa anauza dawa hizo kinyume cha sheria.“Naziuza kimakosa tu maana haziruhusiwi kuuzwa pasipokuwa na kibali cha daktari. Ili umuuzie mtu lazima aje na cheti cha dokta kinachoonesha anahitaji kuzitumia na matumizi yake rasmi ni kwa ajili uchungu endapo mjamzito anataka kujifungua baada ya kazidisha miezi bila kuzaa,” alisema mfamasia huyo bila kujua anazungumza na makachero wa OFM.
Moja ya dawa zinazutumika kutolea mimba ikiwa mkononi mwa kamanda wa OFM.
ENEO LA PILI
Baada ya hapo, OFM ilitua maeneo ya Tandale ambapo ilihitaji huduma hiyo kwenye famasi mbalimbali huku tukio zima likirekodiwa hatua kwa hatua.OFM waliingia kwenye famasi hiyo kwa awamu na kuulizia vidonge hivyo kama vinapatikana na kutajiwa bei ya sh 20,000.

OFM waliomba kupata maelekezo ya matumizi yake ambapo mhudumu mwanamke, alitoa maelekezo:
“Hizi dawa huwa naziuza sana kwa watu mbalimbali kama wanafunzi na wake za watu kwa lengo la kutolea mimba. Vidonge vingine huingizwa sehemu za siri na nyingine unameza. Isipokuwa ukikosea tu kidogo kuziweka zinaweza kuharibu mfumo mzima wa uzazi hivyo unahitajika umakini mkubwa mno.”

Makamanda wa OFM wakichukua maelezo zaidi kutoka kwenye duka hilo la dawa.
ENEO LA TATU
Maeneo ya Magomeni OFM ilibaini dawa hizo zinauzwa sh 15,000 hadi sh 30,000. Hata hivyo, OFM walinunua vidonge hivyo (vielelezo vipo ofisini) kwa bei ya sh 25,000 kwenye duka moja lililopo Magomeni-Kagera.

ZINA MADHARA?
Kwa mujibu wa mtaalam wetu wa afya na uzazi, athari za utoaji mimba kwa kutumia dawa hizo ni pamoja na kuharibu taratibu za kimaumbile kwenye kizazi na kusababisha ugumba.

Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Seif Rashid.
MAGONJWA SUGU
Pia mtoaji mimba huwa na hatari ya kupata magonjwa sugu ya via vya uzazi yanayoathiri shingo ya kizazi na mirija ya mayai. Wanaotumia vidonge hivyo wana uwezekano wa kupata kansa ya uzazi hasa kwa wale wanaoingiza sehemu za siri.

WAZIRI UPO?
Ili kupata mzani wa uchunguzi huo, OFM ilimsaka Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Seif Rashid ili kumjulisha habari hiyo lakini simu yake ya kiganjani haikuwa hewani hivyo jitihada za kumpata zinaendelea.Imeandaliwa na: Mayasa Mariwata, Hamida Hassan, Shani Ramadhani na Gladness Mallya.


0 comments:

-