JUA lilikuwa linakuchwa taratibu katika maeneo haya ya milima ya 
Uluguru pande za Mgeta. Maeneo ya Lukwangule tayari yalishapoteza nuru 
yake ya mchana na kiza kilikuwa kimejivuta kama bibi kizee.
Wakati maeneo hayo kiza kinajivuta maeneo ya kijiji cha lusungi yalikuwa bado yanachechemea na mwanga kidogo uliokuwa unavuka.
kuku
 wote walishaingia katika mabanda yao, wakiwa wametulia tayari kupitisha
 usiku mwingine tulivu. wanyama wa usiku taratibu walianza kutoka katika
 maficho yao, bundi mmoja akaanza kulia.
Katika nyumba moja 
mama kuku alikuwa anahesabu watoto wake huku analia,mbuzi katika mabanda
 walikuwa wanacheua na kondoo nao pia, walikuwa wameshafunguliwa makopo 
midomoni mwao  na wametulia huku beberu mmoja mgomvi akiwa ametiwa kamba
 sawia.
Msichana mmoja mweusi wa wastani, mrefu na ambaye 
alikuwa na umbile la nane, akiwa na mfuko wake mgongoni alikuwa 
anatembea taratibu katika barabara inayoelekea Bumu. Njiani alikuwa peke
 yake, lakini alikuwa anashika kasi ya mtu ambaye hakuwa na mazoea ya 
milima au ambaye ni mgonjwa.
Mwenda binti pekee kwa baba na 
mama Mwenda alikuwa ameondoka nchini miaka saba iliyopita kwenda kusomea
 udaktari nchini Russia. Baada ya kupata vyeti vyake alikuwa na kila 
sababu ya kurejea nyumbani na kuungana na watu wake. Alikuwa amewamisi  
wazazi wake ambao alikuwa na mazoea ya kuwaandikia barua lakini wenyewe 
walikuwa na mazoea ya  kutomjibu.
Alijua kwanini hawataki 
kumjibu. Walimweleza mapema kwamba wanaomba awatumie salamu kila mara 
lakini wao hawataweza kujibu kwa sababu za kiusalama.Walimwambia kwamba 
baba yake mdogo alikufa kwa namna ya ajabu nchini Canada baada ya kusoma
 barua iliyotoka nyumbani akidhani inatoka kwa ndugu zake.
Mzee mmoja mchawi alimuua ndugu yao na akatamba kijiji kizima kwamba amewapatia na hilo hawatakaa walisahau maisha yao yote.
Aliingia
 Dar es salaam saa nne akitokea Nairobi, Kenya ambako aliunga ndege 
yake. Aliunga  mara nyingi sana  usafiri wake kwani alipotoka Moscow, 
alifika Addis Ababa, Ethiopia ambako alikaa kwa siku nzima kabla ya 
kusafirishwa na Ethiopia Airline na kushushwa Nairobi kenya ambako 
alichukua Kenya Airways na kutua uwanja wa ndege wa Dar es salaam saa 
nne asubuhi.
Mpaka saa saba alikuwa amefika kwa ndugu yake 
Magomeni Mikumi katika nyumba ya Uyeka. Aliketi kwa muda kabla ya 
kuondoka kwenda kutafuta usafiri wa Morogoro . Pale kwa shangazi yake 
Magomeni nusura asiondoke baada ya kukutana na wadogo zake ambao 
walishakua wakubwa wakimshangaashangaa.Lakini alipiga moyo konde hasa 
baada ya kuelezwa kuwa wazazi wake hawakuwa katika hali nzuri sana 
inafaa kwenda kuwaona.
Saba nusu, pale Magomeni mapipa alikuwa
 abiria wa mwisho katika Double Coaster moja ambayo haikubeba abiria 
tena mpaka inaingia morogoro saa kumi na nusu. Alifikiria sana kwenda 
gesti kulala lakini aliamua kufanya kitu kimoja cha maana cha kwenda 
katika soko la Morogoro kuona kama hakuna lori linalopandisha kwenda 
kwao Mgeta.
Binti huyu bahati ilikuwa kwake, kwani anatia mguu
 tu akaliona lori ambalo lilikwishapakia pumba na mabati likiwa tayari 
kuondoka.
"Vipi mnapanda mlimani?"
"Ndio bibiye unataka usafiri?"
"Ndio kama inawezekana"
"Utakuwa mwanamke peke yako huko nyuma  manake mbele kumejaa."
"Wala usijali, mpaka Lolo bei gani?"
"Mpaka Lolo? Lolo ndio wapi Hading'oka"
"Ndio Madukani kwani wewe hupajui?"
"Nimechemsha kila mara inakuwa taabu kukumbuka.mama wewe ingia tu tutaelewana sisi binadamu."
"Ninaweza kuwa sina hela hiyo?"
"Huonekani
 kama huna hiyo hela nitakayoihitaji. nataka shilingi 1,500 tu"alisema 
dereva na kisha akamhimiza apande kwani anataka kuingia bado kweupe.
Alifika
  Lolo lakini hakushuka, kwa kuwa lori lilikuwa alinaelekea Tchenzema, 
akashukia visomoro ndipo alipoanza  taratibu hatua za kurejea kwao, huku
 fikira zikimuumiza.
Atawakuta namna gani watu wake na watakuwa vipi. Alikumbuka wadogo zake kutoka kwa mama mdogo wake hakujua atawakuta vipi.
Lakini
 kule nyumbani Baba yake alikuwa amelala akiwa mgonjwa na mama yake 
alikuwa anahangaika  kufanya hiki na kile ili kusawazisha mambo kabla ya
 kuanza kumhudumia mgonjwa wake.
kama vile mtu aliyekwisha 
choka mawazo ya mtoto wake wa pekee yalikuwa yakimjia. Alifikiria mtoto 
wake kwa miaka saba hajawahi kumtia machoni, watu walikuwa wanamdhihaki 
na ndugu wa mume walikuwa wameacha kumsaidia ndugu yao zamani kabisa na 
juhudi kubwa ilibaki kwake yeye ambaye ndiye mke.
Kazi za 
shamba, kazi za kilimo, kazi za kutunza mifugo hazikuwa na msaidizi 
kwani hata wale walio wadogo wanaonekana kama wameambiwa wasifike pale, 
alikuwa anaonekana mchawi anamloga mume wake.
Mama Mwenda 
hakuwa na  muda wa kumsaida mume wake kwa kipindi kile cha jioni ilikuwa
 lazima akimbizane na kutwanga kwanza kabla hajampatia chakula mgonjwa 
wake ambaye hakuonyesha hata dalili za kupona katika ugonjwa wake.
Siku
 ile alimaliza kutwanga mapema akampikia mumewe na baada ya kumkanda kwa
 maji ya uvuguvugu alimnyanyua na kumsaidia kumlisha. Alipoona mgonjwa 
wake yupo safi naye akala na kisha kuanza kujiandaa kwa usiku.
Wakati anafunga mlango kwa kuweka michi na kinu  alisikia hodi ambayo alidhani kwamba ni kichaa chake.
Hodi
 ilirejewa tena na tena na mwisho wake akaamua kuchungulia hakuamini 
aliyemuona pale ndani na badala ya kumfungulia mlango akakimbilia kwa 
mume wake.
"Baba Mwenda, mwenda amerudi" alisema huku akiwa anashangilia.
"Yupo wapi?" aliuliza mzee kwa sauti ya taabu.
"Yupo nje"
"Sasa si kiza kimeingia unawezaje kumwacha nje"
"Ohh
 Mungu ashukuriwe" alikimbilia nje na kuanza kutoa  vifaa alivyoweka 
mlangoni, akafungua mlango na kumkumbatia mwanawe kwa muda mrefu sana 
kabla ya kumsalimia na kumtazmaa kila mahali katika mwili wake.
"Mhh mama hujaacha tu kunikagua kote huko?"
"Mwanangu sijakuona muda gani?"
"Si
 hivi nipo mama." alisema akitabasamu alikuwa anamjua mama yake huwa 
anamkagua hata akitoka shule.Alikuwa na kawaida hiyo kiasi ya kwamba 
alikuwa wakati mwingine anamuona mama yake kuwa kero.
" Wooh 
umekuwa na rangi gani sasa manake bluu si bluu , weusi si weusi rangi 
gani hii" alisema huku akimpokea begi kubwa mgongoni na kwenda kuiweka 
katika chanja ambayo ilitengenezwa vyema kwa ajili ya kuwekea
mizigo.
Aliitazama
 nyumba yao, nyumba iliyomlea. Alitaka kuibadili kama watu wengine 
walivyobadili nyumba za wazazi wao. Alikuwa ameona nyumba nyingi zikiwa 
zimejengwa pau na wala si misonge kama ya kwao ingawa ilijengwa vyema.
Ilikuwa
 nyumba ambayo ina chumba tatu, chumba cha ndani ambacho ni jiko ambako 
kila mara alikuwa akihimizwa kulala humo kutokana na joto lake, chumba 
cha wazazi wake ambacho kilikuwa karibu na zizi la kuku na mbuzi na 
kondooo na kingine ambacho kilikuwa na mwanga na safi kwa ajili ya 
wageni.
Alikumbuka kitanda chake cha teremka 
tukaze ambacho baba yake alikuwa amemnunulia godoro la sufu baada ya 
kupata nafasi ya kwenda shule ya sekondari ya Kilakala kutoka 
Bumu.Ilikuwa taabu kidogo kukumbuka kama mto wake ulikuwa upo au la.
"Mhh
 nambie hali ya baba  mama" alisema huku akiwa amekaa katika kiti cha 
fito kilichokuwa katika sebule ya nyumba yao hiyo ya msonge.Alikuwa ni 
miongoni mwa watoto ambao hawakuwa wanadeka, alikuwa amechangamka na 
mama yake lakini kitendo cha kutomuona baba yake pale akitoka kumuona 
kilimpa shida kidogo, alitarajia habari mbaya manake miaka saba si 
sawasawa.
"Baba yako yupo ndani hali yetu si sawasawa 
mwanangu" alisema kwa huzuni kisha akaanza kumweleza taabu ilianza 
kukohoa na ilipofika kukohoa damu wote waliwakimbia.
"Unaponiona
 hapa sina la kufanya, hatuna hela, hatuna dawa nimekuwa nikihangaika na
 mibaazi mpaka sasa tupo tu. baba zako wamenikimbia mimi sasa ndiye 
muuguzaji." alisema huku anadondosha machozi.
Mwenda aliamka 
na kwenda kumkumbatia mama yake na kisha akaongoza mahali ambapo alijua 
lazima baba yake yupo, chumba cha kati ambacho huwashwa moto.Kweli 
alimkuta baba yake.
Hali ya baba yake ilimtisha.
Alimsalimia na kumuitikia kwa taabu kubwa.
Haikuwa rahisi kuelewa kama anamsikia vyema baba yake au la. Akakimbilia kumbariki kisha akatulia sana.
"Mama ilianza lini?"
"Tunamwaka mmoja" alitulia.
Alimwangalia akatazama mapigo yake kisha akatoka na kukimbilia begi lake.
Ilikuwa taabu kubwa katika moyo wake, alijua baba yake ana kifua kikuu na huenda naye mama yake ana kifua kikuu pia.
 Alienda kuchukua vidonge vya kutuliza maumivu na saplimenti za vitamini.
"Mama baba anakula?" alimuuliza mama yake wakati anaingia tena katika chumba kile.
"Bado anaweza kula japo kwa taabu."
"Basi mpe dawa hizi na kikopo hiki akikohoa tia mate yake." alisema.
"Yanini mama?" aliisikia sauti yake dhaifu.
"Kesho asubuhi asubuhi nataka kwenda kituo cha Afya Mgeta nijue nini."
"Mtaalamu amesema wamemroga kwa sababu wewe upo Ulaya" alisema mama mtu
"Inawezekana mama lakini pia inawezekana baba ana kifua kikuu ndio maana ukimpa mibaazi inatulia"
"Haya
 mama" alisema mama yake na kisha akachukua vidonge vile na kuhangaika 
kumpa mgonjwa na baada ya kumaliza kumpa alikohoa lakini hakutoa  damu 
badaaye alipokohoa alitwaa makohozi na kuona yanadamu na kohosi la 
kawaida. 
Bila hata kujiuliza swali mwenda alitambua kwamba 
nafasi ya baba yake kupona ni hamsini hamsini, kifua kikuu kilikuwa 
kimetafuna sana....
Kwa leo kwaheri tutaonana Jumatatu ijayo kwa mwendelezo
 RSS Feed
 RSS Feed Twitter
 Twitter August 12, 2014
August 12, 2014
 Unknown
Unknown








 
0 comments:
Post a Comment