Monday, November 2

Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), imesema ongezeko la wapigakura limetokana na idadi hiyo kuongezeka baada ya kufanya uhakiki kwenye Daftari la Kudumu la Wapigakura kabla ya Uchaguzi Mkuu.
Kabla ya uchaguzi huo uliofanyika Jumapili iliyopita, katika taarifa yake, tume ilisema jumla ya wapiga kura 23.78 milioni waliandikishwa katika Daftari la Kudumu la Wapigakura kwa mfumo wa Biometric Voters Registration (BVR).
Baadaye tume hiyo ilipochambua taarifa za daftari hilo ilibaini kasoro na kuondoa wapiga kura zaidi ya milioni moja na kubaki na wapiga kura 22.75 milioni.
Daftari hilo lilibaki NEC huku vyama vya siasa vikipewa nakala za daftari kwa ajili ya kumbukumbu zao. Hata hivyo, maswali yaliibuka siku NEC ilipotangaza matokeo ya urais baada ya Mwenyekiti wa NEC, Jaji mstaafu Damian Lubuva kusema watu waliojiandikisha kupiga kura idadi yao ni 23 milioni, idadi ambayo ni sawa na ile ya awali kabla ya wale milioni moja kuondolewa.
Kati ya hao, waliopiga kura walikuwa 15,589,639.
Utata huo umeshalalamikiwa na baadhi ya vyama vya upizani vikiwamo vile vinavyounda Ukawa ambavyo viliitaka NEC kutoa ufafanuzi. Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Habari NEC, Clarence Nanyaro akizungumza na gazeti hili jana, alisema ongezeko hilo limekuja baada ya kupeleka daftari kwenye vituo walikojiandikisha watu kwa ajili ya uhakiki.
Alisema kuna watu waliojiandikisha na walipokwenda kuhakiki majina yao kwenye vituo walivyojiandikisha, hayakuonekana kwenye takwimu za tume.
“Tulifanya uhakiki siku za mwisho karibu na uchaguzi na kubaini kulikuwa na watu wengi ambao majina yao yalikuwa hayaonekani,” alisema Nanyaro
Alisema kutokana muda kuwa mdogo, hawakuweza kutoa nakala nyingine kwa vyama vya siasa kama walivyofanya awali.

0 comments:

-