Wakati joto la urais likizidi kupanda ndani ya CCM kutokana na hofu ya baadhi ya majina mazito ya wagombea wa nafasi hiyo kukatwa kwa mizengwe, vita vya wagombea sasa ni dhahiri baada ya mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM kusema hakuna mtu atakayekatwa bila ya sababu za msingi.
Mjumbe huyo, Sadifa Juma Hamisi, ambaye ni
mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM), pia alisema umoja huo
haujafikia uamuzi wala kumtuma mtu kumdhibiti mwanachama anayetajwa
kuwania urais.
Katika siku za karibuni kumekuwapo mjadala mkubwa
ndani ya CCM juu ya mtu atakayepitishwa kuwania urais kwa tiketi ya
chama hicho, na ilizidi baada ya Rais Jakaya Kikwete kueleza kuwa
mwanachama ambaye atateuliwa na CCM kugombea urais hayumo miongoni mwa
waliojitokeza na kuwataka wanachama kuwashawishi watu wenye sifa
wajitokeze.
Siku chache baadaye, Dk Raphael Chegeni aliliambia
gazeti la Mwananchi kuwa ametumwa na wanachama wa CCM wa mikoa ya Kanda
ya Ziwa kwenda kumshawishi Lowassa kujitokeza kuwania urais kuitikia
wito wa Rais Kikwete wa kuwataka wanachama kuwashawishi watu wenye sifa
kujitokeza.
Hadi sasa, wanachama waliojitokeza kuwania
kuteuliwa na CCM kugombea urais ni Waziri Mkuu Mizengo Pinda, January
Makamba (Naibu Waziri wa Sayansi na Teknolojia), Hamisi Kigwangala, na
Lazaro Nyalandu ambaye ni waziri wa Maliasili na Utalii.
Lakini pia wako wanaotajwa kuwania urais lakini
hawajatangaza ambao ni Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel
Sita, William Ngeleja, Emmanuel Nchimbi, Mwigulu Nchemba, Stephen
Wasira, Bernard Membe na Edward Lowassa ambaye ameibua mjadala kati ya
kambi yake na zinazompinga.
Mapema wiki iliyopita, katibu wa uhamasishaji na
chipukizi wa UVCCM, Paul Makonda alikaririwa akisema kuwa vitendo vyake
vya kumshambulia Lowassa vinatokana na kutumwa na umoja huo kumdhibiti,
jambo ambalo limezidisha mjadala kuhusu mteule wa chama hicho.
Kutokana na hofu hiyo, viongozi wa UVCCM na CCM
mkoani Arusha wametuma ujumbe wa maneno kwa Kamati Kuu na Halmashauri
Kuu ya Taifa za chama hicho wakitaka wanachama wasifanyiwe kile
wanachokiita kuchafuana na vitisho vya baadhi ya wagombea kukatwa
kimizengwe.
Ujumbe huo ulitumwa juzi na mwenyekiti wa CCM wa
mkoa, Onesmo ole Nangole na mwenyekiti wa UVCCM, Robinson Meitinyiku
ambao walitaka Sadifa Juma Hamis kueleza msimamo wa mkoa kwa vyombo
hivyo viwili vya maamuzi, na mjumbe huyo wa Kamati Kuu ya CCM
aliwahakikishia kuwa hakuna mgombea atakayekatwa kwa “sababu za
kijinga”.
Akijibu ujumbe wa viongozi hao, Sadifa aliyekuwa
jijini hapa kumsimika kamanda wa vijana wa wilaya ya Arumeru, Mathias
Manga, aliwaondolea hofu katika hafla hiyo akisema hakuna mgombea wa
urais wa CCM ambaye atakatwa bila sababu za msingi, lakini akawataka
vijana kusubiri zamu yao hadi 2025.
Kauli ya Sadifa
“Niwaombeni mwenyekiti wa mkoa na mwenyekiti wa
UVCCM, msiogope. Hakuna mtu atakayekatwa kijinga ndani ya Kamati Kuu au
Halmashauri Kuu. Kikubwa tufuate maadili. Mimi mchapakazi ndiye
nitamtetea,” alisema bila kutaja mgombea anayekusudiwa.
Alisema ni lazima kiongozi bora awe na mikakati na dira na upeo
wa kuwa na mikakati bora ya kutekeleza ahadi zake kwani hatuwezi kuwa na
kiongozi ambaye hana dira wala mikakati.
“Tunataka kiongozi mwenye kujiamini, awe ana
vision (dira) na mission (mikakati), msikivu... hatuwezi kuchagua rais
ambaye hana sifa hizi,” alisema.
Akizungumzia maombi ya Nangole kuhusu tabia ya
kuwachafua baadhi ya wagombea na kuwatisha, Sadifa alisema hakuna
kiongozi aliyetumwa na CCM na UVCCM kutukana mtu wala kumtisha.
“Mzee wangu, watu wengi wanajua wanamtaka nani,
ukiona mtu anapanda kwenye majukwaa anamchafua mwenzake, ujue huyo ana
mapungufu ya malezi, hakuna haja ya kumjibu kwani utaonekana na pia wewe
una mapungufu,” alisema.
Akionekana kujibu kauli ya Makonda, Sadifa alisema
UVCCM haijatuma mtu amtukane mwingine. Alisema akiwa mjumbe wa Kamati
Kuu, hawajawahi kumtuma kiongozi yoyote kumtukana mwanachama mwingine wa
CCM.
Alipoulizwa kuhusu hofu hiyo, kwa kifupi katibu wa
itikadi na uenezi wa CCM, Nape Nnauye alisema: “Mimi siwezi kuwa
msemaji wa Umoja wa Vijana, nikisema niwajibu nitakuwa nimepotoka.”
Mapema wiki iliyopita, Makonda alikaririwa akisema
kuwa amekuwa akimshambulia Lowassa, ambaye anatajwa kuwania urais
kupitia CCM, kwa sababu ametumwa na umoja huo.
Makonda amekuwa akikaririwa mara kwa mara akisema
kuwa Lowassa hafai kuwa mteule wa CCM wa kuwania urais na mikanda ya
kauli zake imesambaa kwenye mitandao ya kijamii, jambo lililofanya
uteuzi wake kuwa Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni uhojiwe na watu wengi na
hivyo kujikuta akilazimika kusema ametumwa na umoja wake kumdhibiti
waziri mkuu huyo wa zamani.
Katika mazungumzo yake juzi, Sadifa hakutaka
kutaja jina la mgombea atakayemtetea wala mtu anayemshambulia, badala
yake alisema muda ukifika, kila kitu kitajulikana kwa kuwa watu wanamjua
mgombea wanayemtaka.
“Mwenyekiti, dawa ya mjinga ni kukaa kimya, watu
wanamjua mtu ambaye wanamtaka. Rais Jakaya Kikwete ni mtu ambaye
hatabiriki, hana ushemeji... nyie subirini tu wakati ukifika,” alisema.
Vijana na urais
Akizungumzia vijana ambao wanautaka urais, Sadifa aliwataka kusubiri zamu yao hadi 2025 ili wazee waliopo wamalize muda wao.
Alisema utakapofika mwaka 2025 vijana watakuwa katika nafasi
nzuri sana ya kushika uongozi na hawatakubali kuona viongozi wazee
wakitaka kupewa nafasi.
“Wazee tutawaomba radhi mwaka wenu ni 2015 hadi 25, mkimaliza hapo, miaka yenu imekwisha, msije tena,” alisema.
Kauli ya Nangole
Awali, Nangole, ambaye aliwahi kusema kuwa Lowassa
ni kiongozi msikivu na makini na ambaye ni tegemeo la Watanzania katika
kuwaunganisha kuwa kitu kimoja, aliomba Kamati Kuu ipelekewe ujumbe
kuwa CCM mkoani Arusha hairidhishwi na matendo ya baadhi ya viongozi
kuwatukana na kuwatisha wengine.
Nangole alirejea kauli aliyowahi kuitoa kuwa CCM
ni ya wanachama wote na ndani yake hakuna sisimizi au tembo wa kumtisha
mwingine ili mradi anafuata taratibu za chama hicho.
Alisema imeibuka tabia ya baadhi ya viongozi wa
CCM, kuwatisha wengine na kuwatukana kana kwamba wao ndio wana
hatimiliki ya CCM.
Naye mwenyekiti wa UVCCM mkoani Arusha, Robinson
Meitinyiku alisema kuna kiongozi mmoja ametoa kauli kuwa mgombea mmoja
hata kama akisafishwa na madodoki hawezi kuwa msafi.
Badala yake alisema kiongozi aliyetoa maneno hayo
ndiye hawezi kusafishika hata kwa gunzi kwani kuna taarifa aliwahi
kusaliti na kujiunga na chama kingine.
0 comments:
Post a Comment