Thursday, January 22

NYUMA ya ukaribu wa Rais wa Wasafi Classic Baby (WCB), Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’ na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Jakaya Mrisho Kikwete ‘JK’, kuna siri nzito kufuatia mambo mbalimbali yanayojitokeza kati yao kila kukicha, Amani lina cha kukujuza.
Rais wa Wasafi Classic Baby (WCB), Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’ akiwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Jakaya Mrisho Kikwete ‘JK’.
Katika kuunga maelezo hayo, inasemekana kwamba mbali na mambo mengine, hivi karibuni Diamond alimpelekea JK tuzo zake tano za kimataifa alizotwaa mwaka 2014 kwa kuwa nyuma yake kulikuwa na sapoti kubwa ya mkuu huyo wa nchi.
UKARIBU MKUBWA

Kwa mujibu wa chanzo cha karibu ambacho ni ‘mtu’ wa Diamond, staa huyo amekuwa ‘klozdi’ sana na JK kufuatia mambo yake mengi ya msingi kuyafanya kwa kumshirikisha, kiasi kwamba kuna wakati Diamond hata akikurupuka usiku wa manane kama ana jambo huwa hasiti kumpigia simu mheshimiwa na kuongea kwa muda huku wakicheka weee!

IKULU
Habari hizo zilidai kwamba hata kama Diamond akishindwa kuzungumza naye kwa simu, kukicha mguu na njia  hadi ikulu na kuzama ndani kama nyumbani kwao vile ambapo JK akiambiwa anasema ‘mwacheni aingie kijana wangu atakuwa na shida huyo’.

  ‘Diamond Platnumz’ akibadilishana mawazo na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Jakaya Mrisho Kikwete ‘JK’.
“Diamond amekuwa na uhusiano wa karibu kwa kila jambo na JK kiasi kwamba hata yeye anamkubali vilivyo hivyo huwa hasiti kumsapoti pale anapokuwa amekwama na hata kujivunia ukaribu wake na Diamond kutokana na uchapakazi na nidhamu anayoionesha kwake kadiri siku zinavyozidi kwenda.
“Huwezi ukaongea ishu ya muziki na JK asimtaje ‘mwanaye’ Diamond, ukaribu wao umepitiliza na inasemekana wana mikakati mikubwa ya baadaye, ni siri nzito kwa kweli iliyopo baina yao na hakuna anayejua,” kilisema chanzo hicho kwa sharti la kutotajwa gazetini.
SIFA KIBAO
Akizungumza na Amani kuhusu ishu hiyo, Diamond alimmwagia sifa za kutosha  JK huku akithubutu kuanika kwamba, haoni tena katika maisha yake kama atakuja kutokea kiongozi wa juu wa nchi akawa na upendo wa hali ya juu kwa wasanii wa Tanzania kama ilivyo kwa JK.

  Tuzo ambazo Mkali ‘Diamond Platnumz’ alizifikisha kwa Rais Jakaya Kikwete.
“Kiukweli nampenda sana mheshimiwa (JK) na nimekuwa nikijiuliza kila kukicha kama kweli nchi hii tutakuja kupata rais mwenye mapenzi ya dhati na wasanii kama ilivyo sasa kwa baba yetu JK, maana ni mtu wa pekee sana kiasi kwamba muda wowote kama una shida naye yuko wazi kuzungumza na kukupanua mawazo tofauti na unavyoweza kufikiria.
KAMA MWANAFAMILIA
“Mara nyingi siku hizi ninapokutana na rais wetu nimekuwa nikijisikia kama mwanafamilia kutokana na jinsi anavyoniongoza na kuthamini kila kazi inayotokana na muziki wangu jambo ambalo ni la kujivunia sana kwenye maisha yangu maana ninaona wasanii kibao katika nchi nyingine hawafanyiwi haya tunayopata sisi wasanii wa Tanzania kutoka kwa mheshimiwa.

“Nina uhuru mwingi sana wa kuzungumza naye na amekuwa akifanya hivyo karibia kwa kila msanii na kutambua hilo na ndiyo maana hata tuzo zangu nilizopata mwaka 2014 nilimjulisha pamoja na yeye kujua na kunipongeza lakini pia mafanikio hayo naamini yamepatikana kutokana na sapoti yake kubwa ambayo amekuwa akinipatia mara kwa mara.
  ‘Diamond Platnumz’ akiwa katika pozi tofauti na rais wa nchi.
“Sidhani kama kweli tutakuja kupata rais wa aina hii ambaye amekuwa akitambua kila shughuli na fani ya kila Mtanzania maana amekuwa akitujali sana wasanii jambo ambalo halikuwahi kutokea hapo nyuma kwa marais waliopita, husasan kwenye muziki wetu huu wa Bongo Fleva,” alisema Diamond.
MARA YA MWISHO KUKUTANA
Desemba 23, mwaka jana, Diamond alikutana na JK, ikulu ambapo mbali na kumpongeza, walizungumza mambo mengi ikiwemo namna ya kujipanga zaidi kimataifa huku akimweleza madhara ya umaarufu unaendana na kupata mkwanja mrefu.

KUMBUKUMBU ZA HARAKA
Ndani ya makabrasha ya Amani, kumbukumbu zinaonesha kuwa, Diamond ameshakutana na JK si chini ya mara kumi, nje ya nchi na ndani.


0 comments:

-