Monday, April 28



Baraza  la Taifa la Elimu ya Ufundi (Nacte) limesema kuanzia mwaka huu wa masomo, wanafunzi wanaotaka kujiunga na masomo ngazi ya astashahada na stashahada ya utabibu na ualimu, watatakiwa kuomba katika mfumo wa pamoja wa mtandao wa Central Admission System (CAS) na siyo vyuoni kama ilivyozoeleka.
Katibu Mtendaji wa Nacte, Dk. Primus Nkwera, alitoa taarifa hiyo jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki wakati akizungumza na waandishi wa habari juu ya maazimio mbalimbali ya kikao cha 56 cha baraza hilo.

Alisema miaka ya nyuma wanafunzi wa utabibu na ualimu waliotaka kujiendeleza kimasomo, waliomba moja kwa moja vyuoni hali ambayo ilisababisha kuwapo kwa mgongano wa wanafunzi na huku baadhi vikidahili wasio na sifa.

“Mfumo huo utatuwezesha siku ya mwisho ya kuomba waweze kutoa majina waliochaguliwa ili kusiwe na mwingiliano na zoezi hilo litafanywa na Nacte...tumefungua maombi hadi Julai 31, mwaka huu,” alifafanua.

Alisema udahili wa wanafunzi kwa ngazi ya astashahada, stashahada na shahada, umeanza Baraza limetoa usajili wa muda mfupi na mrefu kwa vyuo mbalimbali 17.

Alisema usajili wa kudumu umetolewa kwenye vyuo sita huku usajili wa wa miaka mitano kituo kina uwezo wa kuendesha mafunzo.

Dk. Nkwera alisema usajili wa muda ambao ni wa miaka miwili umetolewa kwa vyuo 11, huku Nacte ikiandaa mitaala 17 itakayotumika kwenye vyuo mbalimbali ili kuepuka kwa vyuo kuwa na mitaala inayojirudia rudia na viwango vinavyotofautiania.

Alisema vyuo viwili vilipata usajili wa maandalizi, haviruhusiwi kuchukua wanafunzi kwa sababu havijafikia kiwango cha kutenda kazi.

“Kwa vyuo vya afya vilivyopewa usajili kabla ya kuanza vinatakiwa kupata mitaala inayotolewa na Nacte na kwenda Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii ili kujiendesha kwa vigezo na masharti ya uendeshaji wa vyuo hivyo.

Vyuo 21 vyafutiwa usajili

Wakati huo huo, katibu huyo alisema vyuo 21 vimefutiwa usajili wake kwa kipindi cha miaka mitatu kutokana na kushindwa kufikia vigezo vinavyotakiwa.

Kwa mujibu wa Dk. Nkwera, kuna jumla ya vyuo 372 na kwamba vilivyofutiwa vilishindwa kujiendedsha kwa mujibu wa sheria na taratibu.

Alisema vyuo vingi vilivyofutiwa vipo jijini Dar es Saalam na vina msongamaono mkubwa wa wanafunzi, kuanzisha kozi zisizo na kibali, kudahili wanafunzi wasio na sifa na kutokuwa na majengo.

Mkurugenzi wa Mafunzo ya Maendeleo ya Rasilimali Watu Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Otilia Gowelle, alisema Mfuko wa Dunia na Taasisi ya Benjamin Mkapa, watatoa udhamini kwa wanafunzi 1,401 na kiasi cha Shilingi bilioni mbili zimetengwa kwa mwaka huu.

Alisema kwa mwaka huu wanatarajia kudahili wanafunzi 6,255 na watakaopewa ufadhili ni wale ambao wataingia mkataba wa kwenda kufanya kazi kwenye maeneo ya vijijini yenye upungufu baada ya kumaliza masomo yao.

0 comments:

-