Friday, October 18


SIRI nzito imetanda juu ya mauaji yaliyotokea hivi karibuni ambapo mama mzazi wa Mtangazaji wa ITV, Ufoo Saro aliuwawa kwa risasi na anayedaiwa kuwa mchumba mtarajiwa wa mtangazaji huyo, Anthery Mushi ambaye pia ni mzazi mwenzake. Mwili wa Anthery Mushi ambaye naye inadaiwa alijiua baada
ya kufanya mauaji hayo umesafirishwa leo kuelekea Uru, Timbirini Mkoani Kilimanjaro kwa mazishi. Bado siri nzito imetawala tukio hilo la kikatili ambalo limesababisha vifo vya watu wawili, yaani mama Ufoo Saro, Anthery Mushi mwenyewe aliyetenda tendo hilo na kujeruhiwa kwa risasi ‘mchumba’ wake (Ufoo Saro) ambaye bado amelazwa Muhimbili kwa matibabu. Tayari ndugu wa Mushi wameanza kuhoji tukio la mauaji kwa mtazamo mwingine baada ya uchunguzi wa maiti kuonekana ndugu yao anayedaiwa kujiua kwa risasi ya kidevu, kukutwa na jeraha la risasi sehemu nyingine mwilini tofauti na ile anayodaiwa kujipiga yeye.
 FAMILIA hiyo imevunja ukimya na kudai kuwa inapata wakati mgumu kuamini kwamba ndugu yao alijiua mwenyewe. Imesema suala hilo inaliachia Jeshi la Polisi lishughulikie ili kubaini undani wake.

Kaka wa marehemu, Isaya Mushi alidai hayo jana alipozungumza na waandishi wa habari katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), wakati mwili wa Mushi, aliyejiua kwa kujipiga risasi na kumuua mama mkwe wake, Anastazia Saro pamoja na kumjeruhi mchumba wake Ufoo, ukiagwa.
Mushi alidai wapo katika wakati mgumu wa kuamini kwamba ndugu yao alijiua mwenyewe, kwani haiwezekani mtu akajipiga risasi sehemu mbili ambazo ni kidevuni na upande wa bega la kushoto.
Alidai sio kazi yao kutoa hukumu, kwani wanasubiri upelelezi wa polisi kutoa jibu lililo sahihi kuhusiana na tukio hilo. Baada ya kifo cha ndugu yetu, wanafamilia tulifanya uchunguzi wa awali na bado linatuwia vigumu kutambua upi ni ukweli kuhusu jambo hilo kuhusiana na kifo hiki,' alidai.
Kaka huyo alidai katika uchunguzi wa madaktari, walibaini kuwa marehemu alijipiga risasi mbili sehemu tofauti. Akisoma historia fupi ya marehemu Mushi, Muhimbili kabla ya kusafirisha mwili huo kuelekea Kilimanjaro kwa mazishi, ndugu wa marehemu, Isaya Mushi ameliomba Jeshi la Polisi kufanya uchunguzi wa busara juu ya tukio zima ili ukweli wa tukio zima ujulikane. Alisema kwa taarifa ambazo wamezipata kulikuwa na kutokuelewana kati ya wapenzi hao yaani Saro na Mushi na ndipo walipolazimika kwenda kwa mama yake na mwanamke na alishindwa kutatua mvutano huo ndipo uamuzi huo mgumu ulifanyika. “Tukio hili ni kubwa sana na sisi limetuumiza sana…manake marehemu alikuwa mtu mpole, mkimya, mwadilifu na mchapakazi aliyekuwa akitegemewa sasa imetustua na uamuzi uliotokea,” alisema msemaji huyo wa familia. “Tunaliomba jeshi la polisi kufanya uchunguzi kwa kutumia busara maana kuna utata wa kauli na matukio halisi. Marehemu amekutwa na majeraha ya risasi mbili, moja inasemekana alijipiga mwenyewe lakini na hiyo ya pili ni utata…sasa uchunguzi ufanywe ili kuondoa utata,” alisema msemaji huyo akizungumza na mtandao huu. Hata hivyo alisema bado kuna utata na ukweli haujulikani hivyo wanaimani labda atakapo pona Saro ataweka wazi juu ya janga zima kwani yeye alikuwa sehemu ya tukio na shahidi namba moja. Aidha baadhi ya ndugu walisema kuna siri nzito juu ya tukio hilo na ukizingatia kwamba Mushi alikuja Tanzania kutokea nje ya nchi alipokuwa kikazi kimya kimya bila hata kumjulisha kaka yake jambo ambalo inaonesha kulikuwa na msuguano kati ya wapenzi hao wawili. “Haiwezekani lazima kuna kitu kimefichika hapa…Mushi alikuja Tanzania kimya kimya kitu ambacho si kawaida yake na ukiangalia baadhi ya vitu alivyokutwa navyo baada ya kutokea kwa tukio hilo unabaini kulikuwa na tatizo kubwa kati ya wawili hawa…tunataka ukweli uwekwe wazi kama kuna dhuluma yoyote imefanywa ijulikane,” alisema mmoja wa rafiki wa karibu wa marehemu Mushi.

Marehemu Anthery Andrew Mushi alizaliwa mwaka 1973 na hatimaye mauti yamemkuta 2013.

0 comments:

-