Thursday, June 26

Kamanda wa Polisi wa Kanda hiyo,Kamisha Suleiman Kova


Kanisa Katoliki Parokia ya Makoka limefichua siri kuhusu mauaji ya Sista Cresensia Kapuli (50), aliyeuawa na majambazi kwa kupigwa risasi kwamba alifikwa na mauti hayo wakati akitoka benki kuweka fedha za sadaka ziliyopatikana Jumapili iliyopita.

Mwenyekiti wa Parokia hiyo, John Bosco Komba, aliliambia NIPASHE jana kuwa sista huyo aliuawa baada ya kutoka benki ya CRDB tawi la Mlimani City kuweka fedha za sadaka na makusanyo ya Shule ya Sekondari ya Mwenyeheri Anuarite.

“Taarifa zilizoripotiwa na vyombo vya habari kwamba ameporwa fedha zinaweza zisiwe na uhakika sana kwa sababu alitoka benki kuweka fedha za makusanyo ya sadaka, ndipo akapitia kununua mchele zaidi ya kilo mbili kwa ajili ya matumizi ya nyumbani kwa hiyo hakuwa na fedha nyingi kama inavyoelezwa na watu,” alisema.
Komba alisema Sista Kapuli mbali na kuwa mhasibu wa shule,pia alikuwa mhasibu wa Kanisa Katoliki Parokia ya Makoka na kwamba siku ya tukio alikuwa na mwenzake Sista Brigitha ambaye ni Mwalimu Mkuu msaidi wa Shule ya Sekondari Mwenyeheri inayomilikiwa na kanisa hilo.
Alisema walipofika katika duka walilokwenda kununua mchele Sista Brigitha ndiye aliyetelemka kwenye gari kwenda kununua na ndipo ghafla majambazi wawili waliokuwa katika pikipiki walitokea na kupiga risasi moja iliyovunja kioo cha gari ambayo ilimjeruhi dereva wa gari hilo, Mark Patrick Mwarabu. 
Aliongeza kuwa majambazi hao walidhani kuwa mkoba aliokuwa nao ulikuwa na fedha nyingi walimpiga risasi mbili Sista Kapuli eneo la titi upande wa kushoto na kufa papo hapo.
Alisema madaktari wa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) wataufanyia uchunguzi mwili wa Sista Kapuli leo kwa ajili ya kumuondoa risasi kabla ya taratibu za kuusafirisha mwili huo kuupeleka kwao katika kijiji cha Mkulwe wilayani Mbozi, mkoani Mbeya.
Alisema baada ya taratibu za uchunguzi wa mwili huo kufanyika, kesho mwili utapelekwa katika Kanisa la Makoka kwa ajili ya misa na kuuaga na safari ya kuusafirisha kwenda kijijini kwao wilaya ya Mbozi itaanza huku akisema kifo hicho kimewasikitisha.
Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, limetangaza kuanza kwa msako ili kuwabaini na kuwakamata majambazi waliohusika katika tukio hilo.
Kamanda wa Polisi wa Kanda hiyo, Kamisha Suleiman Kova, alisema jana kuwa Jeshi lake limeandaa operesheni maalumu itakayohusisha vikosi tofauti ili kuwatia mbaroni wahalifu hao, ambao alisema walipora Sh. milioni 20

0 comments:

-