Jina la Zari hivi sasa limekuwa jina maarufu katika masikio ya Watanzania,
Afrika Mashariki na kwingineko hasa baada ya mwanadada huyo
mfanyabiashara na mwanamuziki wa Uganda kuwa na urafiki na Mwanamuziki
wa Bongo Fleva, Nassib Abdul maarufu kwa jina la usanii Diamond Platnum.
Kwenye mitandao ya kijamii kama Tweeter, Facebook, Instagram na hata
Whatsapp lazima utakutana na jina Zari akiunganishwa na Diamond na
wengine wataunganisha na Wema Sepetu aliyewahi kuwa mpenzi wa Diamond.
Uhusiano kati ya Zari na Diamond umezua gumzo kila eneo Tanzania na
Afrika Mashariki huku wakifananishwa na mastaa wa nje kama vile Kanye
West na Kim Kardashian kwa namna wanavyofuatana wakati wote huku Diamond
akionesha kila aina ya mbwembwe za kumjali mrembo huyo kutoka Kampala,
Uganda.
Uhusiano wa Zari na Diamond umewafanya kuandamana kila sehemu hivi sasa.
Wawili hao walianza kuonekana kuwa na ukaribu wa mahusiano tangu
Diamond alipokwenda Afrika Kusini kwenye Tuzo za Channel O ambapo
Diamond aliibuka na ushindi wa Tuzo tatu.